Kufuatia ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad ya mwaka wa fedha 2017/2018, aliyoiwasilisha bungeni mapema mwaka 2019, iliyoeleza gharama ya utengenezaji wa nembo ya Benki ya TPB, imekuja na sura mpya.

Kufuatia hali hiyo, Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC ) imeiagiza benki hiyo kupeleka mikataba miwili ya zabuni ya utengenezaji wa nembo ya benki kwa ajili ya kupitia baada ya kubaini upungufu.

Akizungumza jana Agosti 21, 2019 Mwenyekiti wa kamati hiyo, Naghejwa Kaboyoka, amesema kuwa lengo la kufanya hivyo ni kuhakikisha mashirika yanafuata sheria ya manunuzi ya umma ili kufanya kazi kwa ufanisi na kuongeza mpato ya Serikali kuu.

”Wanashindwa kutimiza na kusimamia fedha za umma wakijua kuwa watabebwa bebwa tu, wanapaswa kutambua Serikali haitaingilia hilo,” amesema Mwenyekiti wa PAC.

Hata hivyo, ripoti ya CAG ilibainisha kuwa, utengenezwaji wa nembo ya benki hiyo uligharimu kiasi cha shilingi milioni 495, ambapo CAG alisema uamuzi wa bodi ya wazabuni ni wa kutia shaka kwani gharama hiyo ilikuwa na ongezeko la mara mbili ya zabuni ya kwanza iliyokuwa imepitishwa.

Msigwa amgomea RC Hapi, 'Hana mamlaka ya kuniagiza mimi huyo'
Watumishi serikalini watakiwa kutobweteka