Wafanyakazi wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) wameshauriwa kujituma kwa bidii katika kutekeleza majukumu yao ya kazi.
Ushauri huo umetolewa leo na Mtendaji Mkuu wa Temesa Dkt Musa Mgwatu alipokutana na watumishi hao kutoka katika Mikoa/vituo vya Temesa vilivyopo nchi nzima katika kikao kazi kilichofanyika Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.
Dkt Musa Mgwatu amesema kuwa ana muda mchache tangu aanze kutekeleza majukumu yake na ameanza kujifunza mambo mbalimbali kuhusu Wakala huu na kuahidi kupita katika vituo vilivyopo mikoani ili aweze kujifunza zaidi.
“Naahidi kushirikiana nanyi katika kuijenga Temesa Mpya na naomba ushirikiano wenu na muwe wafuatiliaji wa mambo kwani kazi zetu zinahitaji sana ufuatiliaji wa kina” Alisema Dkt Mgwatu.
Ameongeza kuwa amepanga mikakati ya kuiimarisha Temesa katika maeneo ya Matengenezo ya magari kwenye karakana za Temesa, namna ya kuyatambua madeni ya Temesa pamoja na utunzaji wa taarifa zake, utendaji kazi chini ya kiwango wa baadhi ya karakana, mawasiliano kati ya Temesa makao makuu na mikoa au vituo vyake na utendaji kazi na watu au kampuni zilizosajiliwa.
Amesisitiza kuwa watumishi wanapaswa kufanya kazi kwa bidii ili kuondoa dhana potofu iliyojengwa juu ya Temsa kwa wateja wake, wajiimarishe katika utendaji kazi kwa kasi, ubora, weledi uadilifu, ufuatiliaji, na uwajibikaji.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za uendeshaji Temesa Bw. Senzo Gwanchele amesema kuwa kikao kazi hicho kimelenga kuondoa baadhi ya matatizo yanayojitokeza katika utendaji wa kila siku ikiwemo hoja mbali mbali za ukaguzi, ulipaji wa kodi ya ongezeko la thamani (VAT) pamoja na uzingatiaji wa sheria ya Ununuzi wa Umma.
Wakala wa Ufundi na Umeme (Temesa) hivi karibuni imepata Mtendaji Mkuu mpya ambaye amekuja na mikakati ya kujenga na kuimarisha Temesa kwa kupambana na changamoto zinazoikabili Wakala kwa sasa

Aubameyang Afichua Siri Ya Manchester City
Rais Magufuli afanya mazungumzo Ikulu na rais wa congo DRC