Kiungo Mshambuliaji wa Simba SC, Clatous Chama, amewasihi mashabiki wa timu hiyo kuendelea kuwapa moyo wachezaji licha ya kikosi chao kupitia wakati mgumu.

Simba SC hivi sasa imekuwa ikipitia kipindi kigumu, ambapo imeshatolewa katika michuano miwili mikubwa huku katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara ikiwa imepitwa Pointi 12 na kinara Young Africans.

Timu hiyo yenye maskani mtaa wa Msimbazi, Kariakoo jijini Dar es Salaam, hivi karibuni iliaga katika Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika kwa kichapo cha mabao 3-0 dhidi ya Al Ahly ya Misri kabla ya kutolewa na Mashujaa ya Kigoma kwa Penati 6-5 katika hatua ya 16 bora ya Kombe la Shirikisho.

Akizungumzia mwenendo usioridhisha katika kikosi chao, Chama amesema anajua mashabiki wanapitia kipindi kigumu lakini anaamini timu hiyo itarejea katika ubora wake.

Kiungo huyo kutoka Zambia amesema kila mchezaji anajua umuhimu wa kufanya vizuri katika michezo iliyobaki, hivyo wanatamani mashabiki waendelee kuwaunga mkono.

“Hata sisi tunaumia kutokana na kipindi hiki tunachopitia kwa sasa. Ni kipindi cha mpito kwetu, tutakaa sawa na kuendelea kuwapa furaha (mashabiki), kikubwa ni kuhakikisha mashabiki wanatusapoti vya kutosha tuweze kufanya vizuri,” amesema

Simba SC hivi sasa ipo visiwani Zanzibar kushiriki Ligi ya Muungano, ambapo baadae leo Jumatano (Aprili 24) itavaana na KVZ katika Uwanja wa New Amaan Complex.

 

TAKUKURU waibua jipya miradi ya maendeleo Kagera
Mlipuko homa ya Nyani warejea, jamii yatahadharishwa