Mshambuliaji kutoka nchini Serbia na Klabu ya Simba SC Dejan Georgijevic amewataka Mashabiki wa Simba kuendelea kumuamini, kwani amejipanga kuendelea kufunga katika Michezo ya Ligi Kuu.

Dejan alisajiliwa Simba SC mwezi Agosti akitokea Klabu ya Domžale ya nchini kwao Serbia, akipendekezwa na Kocha wa sasa Zoran Maki.

Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 28, amesema anafahamu Mashabiki wa Simba SC wana kiu ya kumuona akifunga na kuiwezesha timu kupata matokeo mazuri.

Amesema kutokana na kutambua hilo, hana budi kuwahakikishia kuwa tayari kufanya kazi wanayoisubiri, na endapo atapewa nafasi na Kocha Mkuu Zoran Maki atapambana na kufikia lengo.

“Kiukweli upendo wa mashabiki wa Simba ni mkubwa ambao wamekuwa wakionyesha kwangu, nawiwa kuwapa furaha kwa kufanya vizuri,” amesema Dejan

Dejan tayari ameshafunga bao moja katika Mshike Mshike wa Ligi Kuu Tanzania Bara, akiifunga Kagera Sugar kwenye mchezo wa Mzunguuko wa Pili uliopigwa Uwanja wa Benjamin Mkapa mwishoni mwa mwezi Agosti.

Hata hivyo Dejan hajawahi kuanzishwa kwenye kikosi cha kwanza cha Simba SC katika michezo ya Ligi Kuu msimu huu, zaidi ya kuwa sehemu ya kikosi cha klabu hiyo kilichocheza mchezo wa Michuano maalum iliyounguruma mjini Khartom-Sudan dhidi ya Al Hilal.

Katika mchezo huo Simba SC ilipoteza kwa kufungwa 1-0 licha ya kukosa baadhi ya wachezaji wao wa kikosi cha kwanza ambao walikuwa kwenye majukumu ya Taifa Stars ambayo imeenda Uganda kwa mchezo wa marudiano (CHAN).

Serikali yahamisha Wanyama kuhofia mabadiliko tabianchi
Jeshi laua raia 50 katika msako wa wahalifu