Rapa wa kike, Rosa Ree amejitoa katika lebo ya The Industry iliyokuwa inasimamia kazi zake za muziki, inayomilikiwa na mtayarishaji wa muziki na mwimbaji, Nahreel.

Mkali huyo wa ‘Up in The Air’ amesema kuwa mkataba wake wa miaka mitatu chini ya lebo hiyo umefikia ukingoni na kwamba pande zote mbili zimeridhia kutosaini mkataba mwingine.

“Mkataba wangu na The industry umekwisha kwa muda huu, lakini napenda kuwashukuru kwa walichonifanyia, ninawashukuru sana kwa kunishika mkono na kunifikisha hapa nilipo,” Rosa Ree ameiambia XXL ya Clouds Fm.

“Hivi sasa nimefika sehemu ambayo naweza kujisimamia mwenyewe, lakini kuna timu kubwa nyuma yangu,” aliongeza.

Rosa Ree alikiri kuwa ingawa hakuondoka The Industry kwa shari, kulikuwa na matatizo kadhaa ambayo waliweza kuyatatua kabla ya kufikia hatua hiyo.

Mkali huyo alitambulishwa na The Industry kwenye kiwanda cha muziki wa Bongo Fleva ambapo alifanya vizuri na kushirikiana na wasanii wakubwa kama Khaligraph Jones wa Kenya.

Uchaguzi wa marudio wapingwa tena Kenya
Florentino Perez amgwaya Harry Kane