Wananchi wakiongozwa na wanaharakati nchini Kenya leo wamefanya maandamano jijini Nairobi kwa lengo la kupinga kukithiri kwa ufisadi nchini humo.
Hata hivyo, wananchi hao waliokuwa wanaongozwa na wanaharakati kadhaa maarufu walilazimika kutimua mbio baada ya jeshi la polisi kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya kwa kufanya maandamano bila kibali.
Waandamaji hao walikuwa wamebeba mabango mbalimbali yanayoshinikiza kukomeshwa kwa vitendo vya ufisadi nchini humo huku wakiwataka viongozi wa nchi hiyo kutangaza mali zao.
Maandamano hayo yalikuwa sehemu ya kampeni maalum ya kupinga ufisadi iliyopewa jina la ‘KnockoutCorrupition’ iliyopata umaarufu zaidi kupitia mtandao wa Twitter.
Baadhi ya waandamanaji walijikuta wakiambulia kipigo kikali kutoka kwa wana usalama.