Mahakama ya Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga, imemuhukumu Makungu Juma (41) kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la kumnajisi mtoto wake wa kambo mwenye umri wa miaka 12.

Hukumu hiyo, imetolewa na Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo Christina Chovenye ambapo alisema adhabu hiyo imetolewa kwa kosa la kubaka kifungu 130 (1) (2)(e) na 131(1) kanuni ya adhabu sura namba 16.

Chovenye alisema kesi hiyo yenye namba 291 ya mwaka 2023 ilifunguliwa baada ya kuletwa shauri hilo mahakamani baada ya kutenda kosa mwezi Julai hadi Septemba mwaka 2023 kwa nyakati tofauti.

Kwa Upande wa shahidi wa kwanza ambaye ni mtoto, alieleza nyakati za usiku alikuwa akimvizia sebuleni akiwa amelala na mdogo wake nakumfanya kitendo cha kumbaka.

Aidha, Hakimu Chovenye alisema shahidi mwingine alikuwa ni kaka yake mtoto huyo ambaye alieleza siku moja alimkuta akifanya kitendo hicho sebuleni ndipo alipokwenda kutoa taarifa kwa mwenyekiti wa kitongoji wanachoishi.

Chovenye alisema, mtoto huyo alikuwa hasomi na kitendo cha kubakwa kilithibitishwa na daktari na kuona sehemu za siri kuharibika vibaya na mahakama imetoa adhabu hiyo ikiambatana kumlipa Sh 500,000 mtoto huyo.

Mke wa mtuhumiwa Makungu alidai wakati mume wake akifanya kitendo hicho hakujua kitu chochote kinachoendelea kufanyika.

Mtuhumiwa Makungun alijitetea mbele ya Mahakama na kukana kuwa hawezi kufanya kitendo hicho kwani ni sawa na mtoto wake na amekuwa akimlea.

Hata hivyo, Wakili wa Serikali ambaye ni mwendesha mashtaka, Evodia Baimo aliomba itolewe adhabu kali kwa mtuhumiwa ili iwe fundisho kwa watu wengine wenye Tania kama hiyo.

Wanawake wa Kiislam wawafariji waliofiwa na wenza wao Hanang'
Makala: Kifo cha kushangaza cha Waziri Mkuu