Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi,Vijana na Ajira), Anthony Mavunde amefanya ziara ya ukaguzi wa masuala ya kazi na kusikiliza kero na changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyakazi mkoani Kilimanjaro.

Mavunde alianza ziara hiyo katika shule ya Kimataifa ya Moshi (ISM) ambapo amesikiliza kero za wafanyakazi na kutoa maagizo kwa Menejimenti ya Uongozi wa Shule hiyo kutoa mikataba kwa wafanyakazi kwa mujibu wa kifungu cha 14 cha Sheria ya Ajira na Mahusiano kazini kinavyoelekeza ikiwa ni pamoja na kuagiza Taasisi za Serikali kuchunguza malalamiko juu ya unyanyasaji kwa wafanyakazi unaodaiwa kufanywa na baadhi ya viongozi wa menejimenti.

Aidha, amewaagiza Afisa Kazi Mfawidhi na Afisa wa Uhamiaji wa mkoa wa Kilimanjaro kuwanyang’anya hati za kusafiria raia 9 wa kichina mpaka watakapowasilisha vibali vya kufanya kazi nchini na vibali vya makazi.

Vile vile, ametembelea Kiwanda cha China Paper Corporation ambapo amesikiliza kero za wafanyakazi na kuiagiza Menejimenti ya Kiwanda hicho kuhakikisha sheria za Kazi zinafuatwa kwa kutoa Mikataba kwa wafanyakazi wote na kuhakikisha haki za wafanyakazi zinalindwa ikiwemo usalama wa mazingira ya kufanyia kazi.

Hata hivyo, Pamoja na maagizo hayo kwa kiwanda,hicho, Mavunde amewataka wafanyakazi nao kutimiza wajibu wao na kutumia njia sahihi za malalamiko yao bila kuvunja sheria za nchi.

Benedictor Tinocco awajibu wanaoibeza Mtibwa Sugar
Baraka Da Prince alia kufanyiwa 'Figisu' YouTube