Meneja wa klabu ya Tottenham Hotspurs Mauricio Pochettino, anaamini kukosekana kwa Chelsea kwenye michuano ya barani Ulaya, ni faida kubwa kwao katika mapambano ya ligi ya nchini England.
Pochettino ameyasema hayo alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu mchezo wa ligi ya nchini England utakaowakutanisha na Chelsea hapo kesho kwenye uwanja wa Stamford Bridge.
Meneja huyo kutoka nchini Argentina, amesema kwa juma zima Chelsea walikua katika maandalizi kabambe ya kujiandaa na mchezo huo, tofauti na kikosi chake ambacho kilikabiliwa na mpambano wa ligi ya mabingwa barani ulaya dhidi ya AS Monaco.
Hata hivyo Pochettino amesisitiza kuwa, hana budi kusaka mbinu mbadala za kukabiliana na changamoto ilio mbele yake, na ana matumaini makubwa kikosi chake kitaingia uwanjani hiyo kesho kikiwa na matumaini ya ushindi.
“Wenzetu Chelsea wana bahati kubwa, hawashiriki michuano ya Ulaya hivyo hupata muda wa kupumzika.
“Kama una timu yenye uwezo mkubwa kama Chelsea na haushiriki michuano ya Ulaya, ni lazima utakua na mwenendo mzuri katika ligi ya nyumbani.
“Chelsea walicheza dhidi ya Middlesbrough siku ya jumapili, na baada ya hapo waligeuzia nguvu zao katika maandalizi dhidi yetu, lakini Tottenham ilipomaliza mchezo wake dhidi ya West Ham United tulifikiria namna ya kujiandaa kuwakabili AS Monaco.” Alisema Pochettino
Michezo mingine ya ligi kuu ya soka nchini England itakayounguruma kesho jumamosi.
Burnley Vs Manchester City
Hull City Vs West Bromwich Albion
Leicester City Vs Middlesbrough
Liverpool Vs Sunderland
Swansea City Vs Crystal Palace
Michezo Jumapili.
Watford Vs Stoke City
Arsenal Vs AFC Bournemouth
Manchester United Vs West Ham United
Southampton Vs Everton