Ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Namungo FC umempa nafasi Kaimu Kocha Mkuu wa Simba SC Juma Ramadhana Mgunda, kuwashukuru Wachezaji wake kwa kazi kubwa walioifanya jana Jumatano (Novemba 16), Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam.

Bao la ushindi la Simba SC lilipachikwa wavuni na Mshambuliaji kutoka nchini Zambia Moses Phiri dakika 31, na kuifanya klabu hiyo kufikisha alaama 24 kwenye msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.

Mgunda amesema wachezaji wake walipambana na kuonesha njaa ya kusaka ushindi kwenye mchezo huo, ambao amekiri ulikua mgumu kutokana na Wapinzani wao kuwa na uwezo wa kupambana na kufanya mashambulizi ya kushtukiza.

“Wachezaji wangu wameonesha kupambana na ndio maana tumefanikiwa kupata alama tatu kwenye mchezo huu, ninaamini walidhamiria kufanya hili tulilipata,”

“Hata wapinzani wetu walifanya kazi kubwa sana kwa kucheza soka lililotupa changamoto wakati wote, walikua shap katika kushambulia kila walipopata nafasi, ila wachezaji wangu walionesha kuwa makini na kuzima kilichokusudiwa dhidi yetu.” amesema Mgunda.

Simba SC itarejea tena Dimbani Jumamosi (Novemba 19) kucheza dhidi ya Ruvu Shooting itakayokua nyumbani Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam.

Majeraha ya Nkunku yampeleka Randal Kolo QATAR
Museveni: 'Lockdown' imesaidia kupunguza Ebola